DKT. NCHIMBI AKOSHWA NA MISIMAMO THABITI YA WANA-CCM PEMBA
Na Mwandishi Wetu,DmNewsOnline
PEMBA ,ZANZIBAR
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi amesema anawaheshimu na kuwakubali wana-CCM wa Pemba kwa misimamo yao thabiti katika kuilinda na kuitetea CCM, bila kuyumba.
Dkt. Nchimbi pia amewapongeza kwa jinsi ambavyo wameendelea kuwa imara kuifanya Pemba kuwa moja ya ngome za Chama Cha Mapinduzi nchini, akiwasisitiza wanaCCM kuendelea kuwa wamoja, chini ya Uongozi wa Mwenyekiti wa CCM, ambaye pia ni Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Katibu Mkuu wa CCM Balozi Dkt Nchimbi amesema hayo leo Machi 23, 2024, alipokuwa akizungumza na baadhi ya viongozi na wanachama wa CCM wa Pemba, waliofika kumlaki katika Uwanja wa Ndege wa Abeid Amani Karume, Pemba, mara tu baada ya kuwasili uwanjani hapo, tayari kuanza ziara ya kikazi ya siku moja, katika Kisiwa cha Pemba.
“Kati ya wanaCCM ninaowaheshimu na kuwakubali sana kwa jinsi wanavyoipenda CCM, wanavyoilinda, kuitetea na kuisemea ni wanaCCM wa Pemba. Asanteni sana kwa mapokezi yenu. "Ameaema
Nakuongeza kuwa "Siku zote mmekuwa imara na daima hamkubali kuyumba. Hongereni sana kwa kuendelea kuifanya Pemba kuwa ngome ya CCM. Leo nimekuja kwa ziara ya siku moja tu, lakini nitakuja ziara nyingine ya kuzungumza na viongozi wote, wanachama wote na wananchi,” amesisitiza Dkt. Nchimbi.
Mapokezi hayo yaliyopambwa na ukaribisho wa kiutamaduni wa CCM, ambapo Katibu Mkuu Balozi Dk. Nchimbi alivalishwa skafu na vijana wa hamasa, mbali ya kuwepo viongozi wa ngazi mbalimbali za Chama na Serikali na wanachama, yaliongozwa na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Ndugu Mohammed Said Mohamed (Dimwa), akiongozana na viongozi wengine, akiwemo Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Mohamed Abood Mohamed na wajumbe wengine wa NEC kutokea Pemba.






Comments
Post a Comment