POLISI IRINGA WATOA WITO WA MSAADA KUWAKAMATA WATUHUMIWA WA MAUAJI YA BENITO
Na Eliasa Ally Iringa,DmNewsonline
IRINGA
JESHI la Polisi Mkoa wa Iringa limewaomba wananchi kushirikiana nalo kwa kutoa taarifa zitakazosaidia kupatikana kwa watuhumiwa wa mauaji ya Benito Avinashi, mkazi wa Wanipogolo, huku likikanusha taarifa zinazosambaa mitandaoni kuhusu kupotea kwa baadhi ya watuhumiwa
Akizungumza na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Alan Bukumbi, amesema kumekuwa na taarifa zisizo sahihi katika mitandao ya kijamii zikidai kuwa Ibrahim Myovela , Asajile Antony, Antony Mwaisaka na Aly Kalolo wamepotea mikononi mwa Polisi ìringa
Kamanda Bukumbi amefafanua kuwa watuhumiwa hao wanatafutwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma mbalimbali za jinai, ikiwemo kuvunja masharti ya dhamana pamoja na kuhusishwa na makosa ya uchochezi kupitia mitandao ya kijamii.
Kwa mujibu wa taarifa ya Polisi, katika hatua za awali za uchunguzi, mtuhumiwa Asajile alikamatwa kwa tuhuma za kuchapisha maudhui ya uchochezi kupitia akaunti ya Facebook iliyotambulika kwa jina la “Mnyakyusa Mpinga Utekaji.”
Baadaye aliachiwa kwa dhamana kwa masharti ya kuripoti Kituo Kikuu cha Polisi Iringa kila baada ya siku tano. Hata hivyo, alishindwa kutekeleza masharti hayo, jambo lililosababisha kuanza kwa msako wa kumtafuta.
Aidha, Ibrahim Myovela anadaiwa kusambaza maudhui ya uchochezi kupitia makundi ya WhatsApp, likiwemo kundi la “M4C Ruaha,” na inadaiwa alibadilisha mawasiliano yake ili kukwepa kukamatwa.
Katika tukio la mauaji, Polisi wamesema watuhumiwa hao wanadaiwa
kumshambulia Benito, ambaye baadaye alifariki dunia kutokana na majeraha aliyoyapata. Inadaiwa kuwa walikamatwa kuhusiana na tukio hilo na kupewa dhamana, lakini hawakurudi kuripoti baada ya kubaini kuwa majeruhi huyo amefariki.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Iringa limesisitiza kuwa linaendelea na uchunguzi na msako mkali dhidi ya watuhumiwa hao, huku likitoa wito kwa wananchi kutoa taarifa zozote zitakazosaidia kukamatwa kwao ili hatua za kisheria ziweze
“Tunawaomba wananchi kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi. Taarifa zozote zitakazotolewa zitahifadhiwa kwa siri,” amesisitiza Kamanda Bukumbi.

Comments
Post a Comment