WAZIRI WA KAIRUKI ATOA MAAGIZO MAZITO KWA TANAPA, ALITAKA KUJA NA UBUNIFU WA KUTANGAZA VIVUTIO VYA UTALII.
Na Mwandishi wetu,DmNewsOnline
ARUSHA
WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Angellah Kairuki ametoa maelekezo mazito kwa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) na kulitaka libadilike ili liweze kuchangia ipasavyo kwenye uchumi wa taifa kupitia utalii na kuhifadhi rasirimali kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye.
Kairuki ametoa maelekezo hayo leo Januari 29,2024 kwenye hafla ya uvalishaji cheo na uapisho wa Kamishna wa uhifadhi,Musa Kuji katika. Kwenye ofisi za Makao makuu ya TANAPA jijini Arusha.
Amesema kuwa katika kipindi hiki Shirika la TANAPA linatakiwa kuja na ubunifu wa hali ya juu katika kutangaza vivutio vya utalii na kubaini mazao mapya ya utalii ili sekta ya utalii iweze kufikia lengo la Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya kuwa na wageni milioni tano na kuliingizia taifa jumla ya dola za kimarekani bilioni sita ifikapo mwaka 2025.
Amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa maono yake ya kuifungua Tanzania duniani kupitia Filamu ya The Royal Tour na kuwataka watumishi wa wizara yake kuchapa kazi ili kuenzi kwa vitendo maono ya kiongozi huyo mkuu wa nchi .
Pia , ameitaka TANAPA kukuza na kuimarisha mahusiano na jamii zinazozunguka hifadhi na mbuga za taifa pia mahusiano na wadau mbalimbali wa hifadhi na utalii ili kuweza kubadilishana mawazo na uzoefu katika uhifadhi na kutangaza vivutio mbalimbali vya utalii duniani pia uendeshaji wa Shirika kwa ujumla wake.
Ameongeza kuwa katika kufanya kazi watumishi wanatakiwa kuzingatia kushirikiana na kufanya kazi kama timu moja huku wakizingatia taratibu za Serikali ili kuweza kupata matokea tarajiwa kwa haraka.
Kuhusu utekelezaji wa miradi ya maendeleo Waziri Kairuki amesisitiza kutekeleza miradi yote kwa wakati huku akisisitiza kufuata taratibu zote za manunuzi ya umma kwa kuzingatia ubora na kuchukua hatua mapema wakati wowote inapotokea changamoto badala ya kukaa kimya na kuruhusu mitandao kuendelea kupotosha.
Katibu Mkuu wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbas amemtaka Kamishna Kuji kuwaunganisha watumishi wote katika kipindi chake huku akimsisitiza kumtanguliza Mwenyezi Mungu.
Hafla hiyo ilipambwa na kikosi maalum cha wanamuziki kutoka TANAPA ambacho kilitumbuiza wimbo maalum wa kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kucheza Filamu ya The Royal Tour.
Comments
Post a Comment