WAJASIRIAMALI WADOGO STENDI YA MAGUFULI WAPATIWA VIZIMBA
Na Mwandishi wetu DmNewsOnline
DAR ES SALAAM
WAJASIRIAMALI wadogo wa Kituo cha Mabasi Stendi ya Magufuli Jijini Dar es Salaam wamekubali kurejea kwenye vizimba walivyopangiwa na uongozi wa stendi.
Akizungumza na waandishi wa habari Mei 7,2026 Jijini hapo,John Shayo mmoja wa wafanyabiashara waliorejea kwenye vizimba kwa niaba ya wenzake amesema kwamba wamekubali maelekeo waliopewa na uongozi wa stendi hiyo
"Sisi kama wafanyabiashara wadogo tuliokuwa tumeweka biashara zetu ndani ya stendi tumekubali maelekezo yaliyotolewa na uongozi kwamba turudi kwenye vizimba kisha huku tuje kwa ajili ya kufanya biashara za kubeba mikononi tu ",amesema
Naye Mwenyekiti wa Jengo la Abiria, Haruna Silanda amesema kurejea kwa wafanyabiashara wadogo kumeleta usawa na mivutano isiyo na tija ,hivyo analishukuru kundi hilo kukubali maelekezo yaliyotolewa na uongozi wa stendi na wameonyesha umoja na mshikamano umerejea.
"Kwetu kama viongozi tumepata faraja kuona wenzetu kukubali kurejea kwenye vizimba na hii itasaidia wao kulipa kodi itakayosaidia kuongeza mapato ya stend,i" amesema
Kwa upande wa mjumbe wa jengo la abiria, Rebeca Bigawa ameiomba serikali kurudisha mabasi ya abiria yanayoanzia sehemu nyingine yarudi stendi kuu ya mabasi ili abiria waweze kuongezeka na wafanyabiashara hao waweze kupata wateja kama ilivyokuwa hapo awali.
"Kwa kweli biashara kwa sasa ni ngumu kutokana na baadhi ya mabasi kuanzia safari zao nje ya stendi kuu na kupelekea kukosekana kwa abiria wengi ndani ya stendi, Ombi letu tunamuomba Rais wetu atuangalie kwa jicho la huruma ili mabasi yote yaanzia safari zake hapa",amesema
Awali ,Meneja wa Kituo hicho cha stendi ,Isaac Kasebo amesema waliweka utaratibu ambao walikuwa wakiusimamia , kupanga wafanyabiashara kukaa kwa utaratibu katika maeneo ya kituo yanayotambulika kisheria.
Alisema katika kutekeleza mpango huo walianza na wafanyabishara ambao walikuwa wanapanga biashara zao katika eneo la kushusha na kupakia abiria ambapo kimsingi walijuwa wanafanya makosa.
Aliongeza kuwa kabla ya kuwaondoa walitoa elimu kufuatia na tangazo muda na sehemu wanayotakiwa kwenda kupata vibanda vyao.
Meneja amesema zoezi lakuwaondoa wajasiliamali hao wadogo ndani ya stendi limefanyika juzi Mei 5, 2026 kuwapeleka sehemu husika kwa kuwapatia vizimba vyao na jambo hilo limekamilika kwa asilimia 100.

Comments
Post a Comment